ASASH GENERAL TRADERS

ASASH GENERAL TRADERS

Thursday, April 3, 2014

SIMBA YAELEKEA KAGERA

SIMBA SC YAENDA BUKOBA BILA TAMBWE, OWINO WAPUMZIKE KWA AJILI YA MECHI NA YANGA APRILI 19

Na Dina Ismail, Dar es Salaam
SIMBA SC imeondoka leo asubuhi mjini Dar es Salaam kwenda Bukoba kwa ajili ya mechi dhidi ya wenyeji, Kagera Sugar Jumamosi, lakini imewaacha wachezaji wake watano tegemeo, wakiwemo beki Mganda Joseph Owino na mshambuliaji Mrundi, Amisi Tambwe.
Mbali na wawili hao, wengine walioachwa Dar es Salaam ni beki Issa Rashid ‘Baba Ubaya’, kiungo Abdulhalim Humud ‘Gaucho’ na mshambuliaji Betram Mombeki.
Yanga watamkoma Aprili 19; Simba SC imeenda Bukoba bila Amisi Tambwe, ili kumpumzisha kwa ajili ya mechi na mahasimu wao wa jadi

Kocha Msaidizi wa Simba SC, Suleiman Abdallah Matola amesema timu imekwenda na wachezaji wengi vijana kwenye mchezo huo ambao wanawaamini watafanya vizuri.
Alipoulizwa sababu za kuwaacha nyota hao watano, Matola alisema; “Hawa wana matatizo ya misuli kidogo, sasa tumeona bora waache wapumzike, kwa kuwa tuna mechi ngumu sana Aprili 19,”alisema kiungo na Nahodha huyo wa zamani wa Simba SC.
Aprili 19, mwaka huu Simba SC itacheza mechi yake ya mwisho ya Ligi Kuu dhidi ya mahasimu wake wa jadi, Yanga SC Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Watacheza watoto; Kocha Suleiman Matola amesema Simba SC imechukua wachezaji wadogo wengi kwa mechi na Kagera Sugar

Simba SC haimo kwenye mbio za ubingwa wala nafasi ya pili katika ligi inayoendelea na imekubali matokeo ikiwa na mikakati ya kujipanga kurudi kwa kishindo msimu ujao.
Yanga SC inapambana na Azam FC na Mbeya City kugombea nafasi mbili za juu kwenye ligi hiyo.  Azam FC inaongoza Ligi Kuu kwa pointi zake 53 baada ya kucheza mechi 23, ikifuatiwa na Yanga SC yenye pointi 46 za mechi 22 na Mbeya City yenye pointi 45 za mechi 23 ni ya tatu.

No comments:

Post a Comment